Sasa haki ya Mungu ipo kwa njia ya Imani katika Yesu kristo kwa wote waaminio.

FANYA UAMUZI SASA!!! Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu (Yesu). Lk 14:27

Name:
Location: Dar Es Salaam, Tanzania

"MUNGU WA BABA YETU IBRAHIM ATUBARIKI"

Wednesday, September 06, 2006

Onyesha Bidii katika maombi

OMBA KWA MUNGU ILI NENO HILI ALILOLITAMKA LITIMIE
Tunakusalimu katika Jina la Yesu Kristo.

Ukisoma kitabu cha Yakobo 5:17,18 utadhani lilikuwa jambo rahisi kwa nabii Eliya kuunganisha kutimia kwa neno alilopewa na Mungu, na kuomba kwake kwa bidii juu ya kutimia kwa hilo neno. Lakini jambo hili halikuwa rahisi kwake.

Tunasoma ya kwamba; “Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinye; na mvua haikunya juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita. Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo ikazaa matunda yake” (Yakobo 5:17,18)

Biblia inasema “akaomba kwa bidii mvua isinye, na mvua haikunya…..akaomba tena, mbingu zikatoa mvua….” Hayo maombi yalikuwa na bidii ndani yake kwa sababu ya hamu kubwa aliyokuwa nayo nabii Eliya kuona ya kuwa neno aliloambiwa na Bwana linatimia.

1 Wafalme 17:1 inasema: “Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Giliadi, akamwambia Ahabu, kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu”

Tunaona ya kuwa hili neno lilitimia.Lakini ili liweze kutimia ilimbidi nabii Eliya aombe kwa bidii au kwa hamu kubwa ya kuona hilo neno alilotamka baada ya kupewa na Bwana linatimia.

Ingawa hatujui nabii Eliya aliombaje, lakini tunajua ya kuwa baada ya kutamka maneno hayo mbele ya Ahabu ilimbidi aliombee hilo neno. Maana tunasoma katika Yakobo 5:17 ya kuwa “….akaomba kwa bidii mvua isinye; na mvua haikunya juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita”.

Baada ya miaka mitatu neno la Bwana likamjia tena nabii Eliya na kusema “Enenda, ukajionyeshe kwa Ahabu; nami nitaleta mvua juu ya nchi” (1 Wafalme 18:1)

Biblia inasema katika 1 Wafalme 18:2 ya kuwa; “Basi Eliya akaenda ili ajionyeshe kwa Ahabu……”

Lakini hata baada ya kujionyesha kwa Ahabu kama alivyoambiwa, bado mvua haikunyesha! Hata hivyo aliambiwa akajionyeshe kwa Ahabu miezi sita kabla ya wakati uliotamkwa wa neno kuwadia!

Hiyo miezi sita ya kusubiri mvua inyeshe kama ilivyotabiriwa ilikuwa ni ya kipindi cha maandalizi makubwa, na ulikuwa muda wa Mungu kusimama upande wa mtumishi wake nabii Eliya mbele ya manabii wa Baali.

Hata baada ya udhihirisho huo mkubwa (1 Wafalme 18:36-40), bado mvua haikunyesha! Nadhani nabii Eliya alikuwa anafikiri ya kuwa, kwa sababu Mungu amesema, basi alilolisema litatimia tu, bila ya yeye kufanya kitu cho chote!

Katika mazingira mengine ni kweli kwamba Mungu anaweza kutamka neno, na akalitimiza, bila ya mtu kufanya jambo lolote. Lakini kuna mazingira mengine, Mungu anasubiri mtu aombe, - tena aombe kwa bidii, ili neno alilolisema alitimize.

Haya ndiyo mazingira yaliyokuwapo wakati wa nabii Eliya. Angalia haya maneno aliyomwambia Ahabu, akasema, “Haya!inuka, ule, unywe; kwani pana sauti ya mvua tele” (1 Wafalme18:41). Hata baada ya maneno hayo, na Ahabu kukubali kuinuka ili ale na kunywa, bado mvua haikunyesha!

Hapo ndipo nabii Eliya alipopata ufahamu ninaotaka na wewe uupate ya kuwa pana uhusiano mkubwa kati ya maombi yako – ukiomba kwa bidii na Mungu kutimiza neno alilolitamka unalotaka litimie au unalotaka lisitimie!

Kwa sababu baada ya kuona mvua hainyeshi, “Naye Eliya akapanda juu mpaka kilele cha Karmeli; akasujudu kifudifudi, akainama uso mpaka magotini” (1 Wafalme 18:42)

Nabii Eliya alikuwa anafanya nini? Nakwambia alikuwa anamwomba Mungu ili atimize neno lake la kuleta mvua baada ya miaka mitatu na nusu kama alivyotabiri! Ndiyo maana imeandikwa, Eliya, “akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake” (Yakobo 5:18)

Ilibidi aombe tena kwa bidii ili mvua inyeshe, na mvua ikanyesha!

Hili ndilo ninalotaka ‘udake’ katika moyo wako ya kuwa, Mungu akisema neno, na una hamu kubwa ya kuona neno hilo linatimia kama lilivyosema, basi unatakiwa uliombee hilo neno kwa bidii zote hadi litimie!

Usifanye kosa kama la nabii Eliya la kudhani ya kuwa kwa sababu Mungu amesema, basi, litatimia tu kama alivyosema, bila ya mtu kufanya jambo! Mazingira mengine ni lazima uliombee hilo neno hadi litimie!

Kwa hiyo, ikiwa una hamu kubwa sana ya kuona maneno ambayo Mungu amenipa kuyasema kwa ajili ya nchi hii, na katika kizazi hiki yanatimia, basi, ni muhimu uyaombee kwa bidii kuanzia sasa hadi uyaone yakitimia!

Unaweza ukasita,- maana si watu wengi wanataka kuweka bidii katika kuomba ili kuona ya kuwa neno la Mungu lililotamkwa kwa ajili yao linatimia! Wengi wangetaka litimie bila ya wao kuomba. Au kama ni kuomba kwa bidii, basi wawaombe wengine wawaombee. Je, una uhakika gani ya kuwa wao wanaokuombea, ni kweli wanakuombea kwa bidii?

Tunaamini Mungu atakujalia kuumalizia mwaka huu wa 2005 vizuri, na pia kukupa fadhili zake zikuingize mwaka 2006 kwa lengo la kuzidi kudumu ndani ya Kristo katika mazingira yote utakayokutana nayo.

Ameni!

Nawambia, vivyo hivyo kuna furaha mbele ya Malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.

NIMESAMEHEWA DHAMBI
ZABURI 32:1-11
Sunday, August 16, 2006
By: Rev. Paul Chisoro


>Dhambi ndiyo sababisho ya huzuni ulizonazo
>Una heri wewe ambaye zoezi la kusamehewa dhambi hufanyika kila wakati
>Hatuwezi kuwa wazuri sana kiasi cha kustahili msamaha wa Mungu
>Kinachohitajika ili upate msamaha ni kuwa na uhusiano na Mungu
>Msamaha ulizaliwa msalabani, Yesu alipokufa akalipa deni lako la dhambi

(A) MAANA YA KUSAMEHEWA DHAMBI

Bwana kusitiri (kufunika) dhambi zako na kuzitupilia mbali au kuzizika kikwelikweli (Zaburi 32:1)
• Kutokukuhesabiwa upotovu, kuondolewa mashitaka au
kuachiliwa huru na Bwana (Zaburi 32:2)

• Kutokuwa na udanganyifu, uongo au hila rohoni mwako(Zaburi 32:2)


(B) KWA NINI NISAMEHEWE DHAMBI?

1) Nisiposamehewa dhambi zangu nitapewa mshahara wake au
malipizi. Warumi 6:23 “ Kwa maana mshahara wa dhambi ni
mauti………....”
NB-Haki ya ki-Mungu inalazimika kuwalipa wenye dhambi
mishahara yao au wadaiwe milele na milele(Ufunuo 20:11-15)

2) Nikisamehewa dhambi nitaitwa heri, yaani aliyebarikiwa.
>Zaburi 32:1,2 “Heri”, yaani amebarikiwa kiasi cha kuonewa
wivu, ana bahati njema au ana furaha isiyoneneka,
aliyesamehewa dhambi zake
>Warumi 6:23 “bali zawadi ya bure ya Mungu ni Uzima wa
milele kupitia kuungana na Yesu Kristo Bwana wetu

3) Nahitaji uhusiano mzuri na Mungu wangu.
>I Petro 2:24..Mungu aliweka maovu yangu yote juu ya
Kristo, akawa sadaka ya dhambi

4) Nikisamehewa dhambi, Bwana atanifundisha na kunielekeza
njia nitakayoiendea na atanishauri huku jicho lake likinitazama
(Zab.32:8)

5)Maji makuu ya majaribu yakifurika hayatanifikia(Zaburi 32:6-7)


(C) KWA NJIA GANI NAWEZA KUSAMEHEWA DHAMBI?

1) Nitambue ugumu wa maisha ya kuishi na dhambi
zisizosamehewa.
>Zaburi 32:3-4..maneno haya, mifupa yangu ilichakaa, mkono
wako ulinilemea(wa kutopendezwa nami), na jasho langu
lilikauka hata nikawa kama nchi kavu, hufafanua ugumu
wa maisha wa mtu asiyesamehewa dhambi.

2) Nimjulishe Bwana dhambi zangu bila kumficha.
>Zaburi 32:5“Nimjulishe Bwana dhambi zangu bila kumficha
upotovu wangu na kukiri maasi yangu kikamilifu hadi yote ya
nyuma yasemwe kwake

3) Niombe msamaha wa dhambi.
>Zaburi 32:6-Niombe msamaha huu wakati Bwana anapatikana
na kwa kuzingatia kwamba Yeye ni mwingi wa rehema

NB. Tofautisha kumjulisha Bwana dhambi yako na kuomba
msamaha wa dhambi. Baada ya kumjilisha dhambi zako
inabidi uombe msamaha wa hizo dhambi.

4) Kwa kuwasamehe wengine walionikosea (Luka 11:4)
>Marko 11:25-26…Nisipowasamehe wengine makosa yao ,
Baba wa mbinguni hatanisamehe na mimi dhambi zangu

ZINGATIA-ZABURI 130:3-4
Zaburi 130:3 “ Bwana kama wewe ungehesabu maovu, na
kututendea sawasawa na dhambi zetu, ni
nani angesimama? ”

Zaburi 130:4 “Lakini kwako kuna msamaha (ambao ndio
tunaouhitaji mwanadamu) ili upate kuogopwa
na kuabudiwa”